Tuesday, May 28, 2013

MAHAKAMA YAONDOA HATI YA KUKAMATWA KWA MAKUNGA

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imemwondolea Meneja Uendelezaji Biashara wa Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd (MCL), Theophil Makunga, hati ya kumkamatwa.

Hakimu Mkazi, Warialwande Lema, juzi alitoa amri ya kumkamata Makunga na kumfikisha mahakamani, baada ya kuchelewa kufika kortini kuhudhuria kesi ya kuchapisha makala inayodaiwa kuwa ya uchochezi inayomkabili yeye na wenzake wawili.
Hata hivyo, Mahakama hiyo jana ilimwondelea hati hiyo baada ya kujisalimisha mwenyewe na kujieleza sababu za kutowahi wakati kesi hiyo ikitajwa.
Makunga alidai kuwa hakudhamiria kutofika mahakamani, bali alichelewa kwenye foleni.
Akizungumzia hatua ya kumwondolea hati ya kumkamata, Makunga alisema amefurahi na anashukuru kwa uamuzi huo.
Kesi hiyo ilitajwa juzi, lakini hadi wakati mahakama inaanza, Makunga alikuwa hajafika mahakamani.
Wakili wake, Frank Mwalongo alidai kuwa mteja wake alikuwa njiani na kwamba, alikuwa amekwama kwenye foleni.
Hata hivyo, Wakili wa Serikali, Lilian Itemba aliomba Mahakama itoe amri ya kumkamata mshtakiwa, ombi ambalo Hakimu Lema alilikubali.
Kesi hiyo iliahirishwa hadi Juni 20, mwaka huu, itakapotajwa tena mahakamani hapo. Makunga ni mshtakiwa wa tatu aliunganishwa kutokana na gazeti la Tanzania Daima, kuchapishwa kwenye kiwanda cha MCL.

No comments:

Zilizosomwa zaidi