Wednesday, May 7, 2014

GONJWA HATARI LAITIKISA DAR.....



Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imetoa tamko kuwa ugonjwa wa homa ya dengue umefikia hatua mbaya.
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid alisema jana kuwa kuna hali ya hatari na maambukizi ya ugonjwa huo yanaongezeka, hivyo wananchi wanatakiwa kuwa makini.
“Kwa ufupi, mbu sasa ni hatari kuliko ilivyokuwa awali kwa sababu hawa wanaoambukiza homa ya dengue huuma wakati wa mchana, tofauti na wale wanaoambukiza malaria ambao huuma usiku na watu walikwishajua kujikinga kwa chandarua au dawa,” alisema.
Waziri Rashid aliwataka wananchi kuchukua hadhari kwa sababu ugonjwa huo hauna chanjo wala tiba... “Kila mtu anatakiwa kuchukua hatua, maji yasiruhusiwe kutuama kwa muda mrefu kwani humo ndimo mbu huzaliana kwa wingi. Kwa mfano, maji yanayotuama kwenye kofia za mabati, kwenye vifuu na kwenye madimbwi yanatakiwa yaondolewe ili kuzuia mbu hao.”
Alisema ni vyema watu waende hospitali kupima badala ya kuuchukulia kila ugonjwa kuwa ni malaria na akawataka wasipende kutumia dawa kwa matakwa yao kabla ya kuonana na daktari.
Daktari Mtafiti katika Kliniki ya Shule ya Kimataifa ya Tanganyika (IST), Belia Klaassen alisema tangu Januari mwaka huu hadi jana, watu waliogundulika kuambukizwa dengue ni 203, kati yao 110 waliugua Aprili pekee.
Alisema tatizo hilo linaongezeka kwa kuwa kuna wagonjwa 20 wapya wanaogundulika kila siku.
NIMR kufanya utafiti
Mkuu wa Kitengo cha Utafiti cha Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), Dk Julius Massaga alisema: “Upo uwezekano wa kufanya utafiti wa tiba ya ugonjwa huo. Kwa ufupi, huyo mbu anayesababisha homa ya dengue yupo hata hapa kwetu NIMR, kwenye mazingira yetu.”
Dengue ilianzia IFM
Tukio la kwanza katika mfululizo kugundulika kwa maradhi hayo lilibainika miaka mitatu iliyopita baada ya wanafunzi kadhaa wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), kufariki dunia mfululizo.
Daktari Kiongozi wa Hospitali ya Mwananyamala, Mrisho Rupinda alisema jana kwamba wagonjwa hao walibainika mwishoni mwa 2011 na baada ya uchunguzi wa awali ilibainika kuwa idadi kubwa waliathiriwa na dengue.
“Kwa wakati ule, wataalamu wengi walikuwa hawajajua kuwa ugonjwa huo umeingia. Waliwapima vipimo vya kawaida na baada ya kutoona vijidudu kama vya malaria waliwatibu kwa utaalamu wa kawaida, baada ya vifo kadhaa ndipo ilipobainika kwamba kulikuwa na tatizo lisilokuwa la kawaida,” alisema Dk Rupinda.
Katika hatua za awali, wataalamu walitumwa kunyunyiza dawa kwenye eneo lote la chuo hicho na kwenye hosteli za wanafunzi wake zilizopo Kigamboni.
Baada ya hatua hiyo, ndipo Kituo cha Utafiti wa Magonjwa (CDC) cha Marekani kupitia kitengo chake cha uchunguzi wa magonjwa kilipotuma wataalamu ambao kwa kushirikiana na wataalamu wazalendo, walibaini ugonjwa huo.
Ray C apata ruhusa
Mwanamuziki Rehema Chalamila ‘Ray C’, ametoka katika Hospitali ya Mwananyamala, Dar es Salaam alikokuwa amelazwa kwa maradhi hayo.
Akizungumza kwa simu jana, Ray C alisema ameondoka hospitalini na yuko nyumbani baada ya kuruhusiwa na madaktari.
Mganga Mkuu wa Hospitali hiyo, Dk Sophinias Ngonyani alisema mwanamuziki huyo aliruhusiwa baada ya kupata nafuu na hali yake kuonekana nzuri.
Chanzo: Mwanachi

No comments:

Zilizosomwa zaidi