
Mwanamuziki mashuhuri nchini
Rwanda pamoja na mwanahabari mmoja wamekamatwa kwa tuhuma za kuwa na
uhusiano na kundi la upinzani pamoja na kushirikiana na waasi.
Kwa mujibu wa polisi ,Cassien Ntamuhanga ambaye
ni mkurugenzi wa, kituo cha redio ya kikristo alikamatwa Jumatatu huku
mwanamuziki Kizito Mihigo akikamatwa mnamo Ijumaa.
Wawili hao wanatuhumiwa kuwa na uhusiano na chama cha kisiasa cha (RNC) kilicho na makao yake nchini Afrika Kusini.
Pia wanadaiwa kuwa na uhusiano na waasi wa Hutu walio katika nchi jirani ya DRC.
Chama cha RNC kiliundwa na Patrick
Karegeya,aliyepatikana akiwa amefariki katika hoteli moja nchini Afrika
Kusini mapema mwaka huu.
Washirika wake pamoja na familia yake wanalaumu serikali ya Rwanda, kwa mauaji yake madai ambayo Rwanda imekanusha vikali.
Polisi wadai kuwa wawili hao pamoja na aliyekuwa
mwanajeshi Jean Paul Dukuzumuremyi, walipanga mashambulizi ya kigaidi
kwa lengo la kupindua serikali na kuwaua maafisa wa serikali na pia
kuchochea ghasia.
Wanadaiwa kushirikiana na waasi wa FDLR ambao
baadhi ya viongozi wao walishiriki katika mauaji ya kimbari ya mwaka
1994 ambapo watu 800,000 wa kabila la Tutsi na wahutu wenye msimamo wa
kadri waliuawa.
Inaarifiwa bwana Mihigo alikuwa na uhusiano wa karibu na chama tawala cha (RPF),na kwamba kukamatwa kwake kumewashangaza wengi.
Rais Paul Kagame aliingia mamlakani punde baada ya mauaji ya kimbari kumalizika.
Wengi wamemsifu kwa kukuza uchumi wa nchi hiyo huku baadhi wakimlaumu kwa kukandamiza uhuru wa watu kujieleza.
CHANZO: BBC
No comments:
Post a Comment