Friday, October 25, 2013

YANGA WAAHIDI USHINDI KWA KWENDA MBELE

Kikosi cha Yanga
          Kikosi cha Yanga                                    
Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Bara, Yanga wamesema kwa sasa wanajipanga na mchezo wake ujao dhidi ya Mgambo Shooting ambapo imeahidi kuendeleza mvua ya magoli.
Wakati Yanga ikitamba hivyo, Simba nayo imepania kuifunga Azam katika mechi yake itakayochezwa Jumatatu. Yanga katika mchezo wake uliopita uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam iliiadhibu timu ya Rhino Rangers kwa magoli 3-0.
Yanga itaumana na Mgambo Shooting Oktoba 29 mchezo ambao awali ulikuwa uchezwe kesho na ulisogezwa mbele kupisha mchezo kati ya Timu ya Wanawake ya Tanzania chini ya umri wa miaka 20 na ile ya Msumbiji katika mchezo wao wa kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia kwa Wanawake wa umri huo.
Akizungumza jana, Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kiziguto alisema timu yake iko katika hali nzuri na kama ilivyokuwa katika mchezo wao uliopita ndio ambavyo watafanya katika mchezo ujao.
Alisema kuwa Yanga imejipanga kuhakikisha kuwa inaongoza kwa pointi katika ligi na kuongeza kuwa itahakikisha inatetea taji.
“ Kwa sasa wachezaji wapo katika hali nzuri ya kimchezo na wachezaji wote wana nia ya kuwapa raha wapenzi wa klabu hivyo basi watu wangojee ushindi,”alisema Kiziguto.
Kwa upande wa Simba ambao kwa sasa wana pointi 20 wakiwa sambamba na Azam pamoja na Mbeya City wametamba kubadilisha matokeo ya sare watakapokutana na Azam.
Simba ilitoka suluhu na Coastal Union juzi, ikiwa ni sare ya pili mfululizo baada ya kutoka sare ya mabao 3-3 na Yanga. Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga ameahidi ushindi katika mchezo huo.
Alisema kuwa wachezaji wapo katika hali nzuri ya kimchezo na kuongeza kuwa itakuwa ni fursa yao ya kujiimarisha zaidi kileleni katika mchezo huo.
“Ni imani yangu kuwa mchezo huo utakuwa mzuri na wapenzi wa Simba waje wajionee namna ambavyo vijana wao wanafanya kweli na kuiongezea pointi tatu na kuwa na pointi 23,” alisema.
Chanzo: Habari Leo

No comments: