Sunday, May 26, 2013

HII NI RIPOTI MAALUM KUTOKA GAZETI LA MWANANCHI: WAZAZI WANASINGIZIA WATOTO WAAO WAMEFARIKI ILI KUWATOA SHULE NA KUWAOZESHA

Wazazi wilayani Mkuranga  wamebuni mbinu mpya ya kuwaachisha shule watoto wa kike, ambapo wanashirikiana na baadhi ya walimu kuandika ripoti za uongo kwamba mabinti hao wamefariki dunia.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa baada ya wazazi kubanwa na Serikali wanapowaachisha mabinti zao shule kwa lengo la kuolewa, wengine wamebuni mbinu za kusingizia vifo kwa mabinti hao.
Kwa mujibu wa uchunguzi gazeti hili kuna idadi kubwa ya wanafunzi wa kike katika shule za sekondari na msingi, ambao wameacha shule baada ya kupata ujauzito na wengine kuolewa.
Taarifa za uchunguzi zilibaini katika shule za sekondari za Kizomla na Mgulani zaidi ya wanafunzi ishirini (majina tunayo) walipata ujauzito na watano waliolewa kati ya mwaka 2009 na 2012.
Akizungumzia utoro na upungufu wa wanafunzi shuleni hapo, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Frank Mjenga alisema kuwa wanafunzi wanazidi kupungua kutokana na utoro, kupata mimba pamoja na kukosekana kwa mazingira rafiki kwa wanafunzi.
“Hawa wanafunzi wanapungua kwasababu ya uzembe…kwa mfano mwaka huu nimepewa wanafunzi 18 tu, darasa linatakiwa kuwa na wanafunzi 40,” alisema Mjenga.
Mkazi wa kijiji cha Mgulani, Jafari Jongo alisema kuwa kuna wazazi ambao wanashirikiana na walimu kuwatorosha wanafunzi na kuwaoza kwa kutumia njia mbalimbali kuficha ukweli.
“Imetokea mara mbili hapa katika Shule ya Msingi Mgulani, wazazi walishirikiana na walimu kuwaozesha wanafunzi halafu wakaandika kuwa wanafunzi hao walifariki dunia, ili viongozi wa juu wasifuatilie,” alisema Jongo.
Kwa mujibu wa Jongo ‘mchezo’ huo hufanywa kwa ushirikiano mkubwa kati ya walimu na wazazi ambao huwasafirisha wanafunzi walioolewa na kwenda kuwaficha katika vijiji vya mbali.
Naye Mariam Amrani mkazi wa Mgulani, akizungumzia tatizo la kuwazushia vifo mabinti kwamba aliwahi kusikia walimu wakifuta jina la mwanafunzi wa kike, kwa maelezo kwamba amefariki dunia.
Kauli ya walimu
Mwalimu Frank Manonge ambaye anafundisha Kemia katika Shule ya Sekondari Kizomla alisema kinachosikitisha zaidi ni namna baadhi ya wazazi wanawachukia walimu ambao wanapambana na vitendo vya kuwaoza wanafunzi.

“Tumeshuhudia wanafunzi wakipata mimba na wengine wakiolewa na kuacha masomo, lakini kitu cha kushangaza baadhi ya wazazi wanavifurahia vitendo hivyo kwa kuwafanyia sherehe wanafunzi wanaoolewa huku wakiwaachukia walimu wanaopinga ndoa hizo,” alisema Manonge.
Manonge alisema kuwa katika moja ya mikutano ya shule, mzazi mmoja alisimama na kuwafokea walimu kwa vitendo vyao vya kufuatilia watoto wa kike, wanapotoroshwa shule na kupelekwa kuolewa.
“Tuliwahi kushiriki kikao mzazi mmoja alisimama na kuwatisha walimu wanaofuatilia masuala ya mapenzi kwa wanafunzi. Akisema “yanawahusu nini mambo yao,” alisema mwalimu Frank Manonge.
Mwalimu anayefundisha katika Shule ya Msingi Mgulani ambaye hakutaka jina lake kuandikwa gazetini kwa kuhofia usalama wake, alisema habari kuhusu kuwepo kwa taarifa za mwanafunzi kuandikwa kwenye kitabu cha orodha cha wanafunzi kuwa alifiriki ili kwenda kuolewa zilienea kijijini lakini si za kweli kwa kuwa hakuna anayeweza kuthibitisha.
“Taarifa hizo zimekuwepo kijijini hapa na hivyo ndivyo inavyoaminika, lakini hakuna mtu anayeweza kuzithibitisha kwa kuwa imebaki kuwa siri kati ya wahusika,” alisema mwalimu huyo na kuongeza kuwa ni kweli wazazi wanashiriki kuwaoza binti zao.
Akizungumzia tatizo la wanafunzi kuolewa na wengine kupata mimba, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Kizomla, Frank Mjenga alisema wanafunzi wengi wanapata mimba kutokana na utamaduni wa wakazi wa wilaya hiyo wa kuwacheza ngoma watoto wakiwa bado wana umri mdogo na hivyo kuchochea kufanya vitendo vya ngono.
Akizungumzia utoro na upungufu wa wanafunzi shuleni hapo, Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Frank Mjenga alisema kuwa wanafunzi wanazidi kupungua kutokana na utoro, kupata mimba pamoja na kukosekana kwa mazingira rafiki kwa wanafunzi.
“Hawa wanafunzi wanapungua kwa sababu ya uzembe…, kwa mfano mwaka huu nimepewa wanafunzi 18 tu, darasa linatakiwa kuwa na wanafunzi 40,” alisema Mjenga.
Francis Gewe ambaye mwanafunzi wake anasoma katika Shule ya Msingi Mgulani, alisema kama hatua za haraka hazitachukuliwa kudhibiti vitendo vya wanafunzi kupata mimba na kuolewa itafika wakati wazazi hawatawapeleka wasichana shuleni.
“Ukigeuka huku huyu binti yake kapata mimba, mwingine kaolewa. Itafika wakati wazazi wataona haina muhimu kuwapeleka shuleni watoto wa kike,” alisema Gewe.
Kauli ya Serikali
Akizungumzia suala hilo, Ofisa Elimu Utawala, Wilaya ya Mkuranga, Elizabeth Ngonyani alisema kuwa tatizo hilo limekuwa kubwa kutokana na wazazi wengi kushindwa kutoa ushirikiano kwa serikali za vijijini wakati wanapotakiwa kutoa taarifa kuelezea kwa nini watoto wao wameacha masomo. “Binti anabainika kuwa ameacha shule tena ni mjamzito, lakini ukimuuliza anasema nilikutana na kijana mmoja kwenye gulio akanipa mimba.

Ukweli ni kwamba wazazi wanashirikiana na mwanafunzi kuficha taarifa,” alisema Ngonyani na kuongeza kuwa: “Kama ungetupa taarifa mapema tungekuandalia orodha ya wanafunzi waliopata mimba.”
Ngonyani alibainisha kuwa kutokana na vitendo vya wazazi kutotaka kusema ukweli, Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Henry Clemence aliwaonya wazazi ambao watoto wao wamekatiza masomo bila sababu za msingi kuwa wataanza kuchukuliwa hatua za kisheria.
“Tatizo ni kubwa sana kiasi kwamba kuna wakati Mkuu wa Wilaya alitaka wazazi waanze kuchukuliwa hatua za kisheria,” alisema Ngonyani.
Hata hivyo, Diwani wa kata ya Mkamba, Hassan Dunda alisema kuna wazazi ambao walifikishwa katika mabaraza ya kata baada ya watoto wao kupata ujauzito na kuolewa, lakini kesi hizo zinachukua muda mrefu kutolewa uamuzi kitu kinacholalamikiwa na wananchi.
“Kwa kawaida mzazi ndiye anayetakiwa kumshtaki mtu aliyempa mimba binti yake, lakini huku wazazi ‘wanamalizana’ na mhusika. Hata hivyo wale waliofikishwa kwenye mabaraza ya kata kesi zao zinachukua muda mrefu mno,” alisema Dunda.
Akizungumzia namna tatizo la wanafunzi kupata ujauzito lilivyo kubwa, Dunda alisema kuwa binti wa mdogo wake aliyekuwa anasoma Shule ya Sekondari Kizomla aliacha masomo baada ya kupata ujauzito na kwamba bado yupo nyumbani anasubiri kujifungua.
Wazazi na wanafunzi wanasemaje?
Mkazi mmoja wa Kijiji cha Mkamba Tungi, Salama Saidi, ambaye binti yake alipata ujauzito na kujifungua wiki kabla ya kufanya mtihani wa kidato cha nne mwaka 2012, alisema tatizo la mimba ni kubwa kiasi kwamba jamii inayomzunguka haishangai.
“Hapa hakuna mtu anayeshangaa mwanafunzi kupata ujauzito, ila wapo wachache ambao wanajua namna nilivyomsomesha binti yangu kwa shida, hao ndio wanaonionea huruma,” alisema Salma.
Aliongeza: “Namshukuru Mungu mjukuu wangu na mwanangu wanaendelea vizuri.”
Mwanafunzi Omari Mohamed aliyekuwa kidato kimoja na binti ya Salma (jina tunalihifadhi) alisema wanafunzi walipata shida kusoma na mwanafunzi mjamzito.
“Tulimshangaa baadaye tukamzoea kwa kuwa kila mtu alikuwa anajua kuwa yeye ni mjamzito, lakini aliendelea kuja darasa hadi alipojifunga siku chache kabla ya kufanya mtihani,” alisema Mohamed.

Taarifa zilizopatikana katika kijiji cha Kimanjichana zimebaini kuwa wazazi huwatoza vijana wanaooa wanafunzi kati ya shilingi laki moja na tatu.
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa Shule ya Sekondari Kizomla ndiyo iliyoathirika zaidi na tatizo la watoto kuacha masomo kwani tangu kuanzishwa kwake mwaka 2009 imekwisha wasajili wanafunzi 254 kati ya hao wanafunzi 127 wameacha masomo kutokana na sababu mbalimbali.
Kati ya wanafunzi 100 walioingia darasa la kwanza mwaka 2009 waliomaliza kidato cha nne ni 72. Mwaka 2010 walisajiliwa wanafunzi 77 ambao hivi sasa wamebaki 33, huku kidato cha pili walioanza 35 wamebaki 20 tu.

No comments:

Zilizosomwa zaidi