Wednesday, September 11, 2013

HII NI YA MIKOA YA DAR NA ARUSHA KUKABILIWA NA NJAA, KIGOMA, MBEYA, KAGERA, IRINGA SHANGWE TUPU

Mikoa mitano nchini inakabiliwa na uhaba wa chakula na serikali imesema inajipanga kufanya tathmini itakayobainisha hali halisi. Tathmini hiyo inayotarajiwa, itaangalia ni kwa kiwango gani sanjari na kaya zilizoathirika katika mikoa hiyo ya Arusha, Dar es Salaam, Manyara, Shinyanga, Simiyu na Tabora.
Mkurugenzi wa Usalama wa Chakula nchini, Karimu Mtambo alitoa taarifa hiyo jana Dar es Salaam kwenye warsha iliyoandaliwa na mradi wa unaoangalia juu ya usalama wa chakula ujulikanao Sera.
Hata hivyo, Mtambo alisema ipo mikoa mingine yenye chakula cha kutosha kutokana na kuzalisha ziada. Nayo ni Rukwa, Katavi, Ruvuma, Mbeya, Kigoma, Iringa, Kagera, Mtwara, Lindi na Morogoro.
“Takwimu hizo ni za awali ambazo tumezipata juzi jioni ingawaje bado serikali itafanya tathmini ya kina kuona maeneo hayo yameathirika kwa kiwango gani na kaya ngapi ambazo zitakuwa zimekosa chakula,” alisema Mtambo na kuongeza kuwa mikoa mingine, imezalisha kwa kiwango cha kujitosheleza.
Mradi huo unaoendeshwa na Shirika la Marekani la Feed the Future chini ya udhamini wa Shirika la misaada la Marekani (Usaid), ulikuwa ukiwasilisha utafiti mbalimbali kuhusu usalama wa chakula.
Katika warsha hiyo, Mtambo alifafanua kwamba uwiano wa kiwango cha njaa kwa mikoa hiyo kinatofautiana.
Tathmini hiyo imeonesha kiwango ambacho kiko chini ya asilimia 100 huku ikiwepo mikoa ambayo imezalisha zaidi hadi asilimia 120.
Alisema katika tathmini itakayofuatia wataungana na wadau mbalimbali kujua watu walioathirika na wanahitaji chakula kiasi gani. Kuhusu hali ya ghala la taifa alisema lengo lilikuwa kuhifadhi chakula tani 250,000 na kwamba hadi kufikia sasa zipo tani 185,000 za nafaka.
Akizungumzia mradi wa SERA, Mshauri Mwandamizi wa Sera za Kilimo, Alex Mkindi alisema unawasilisha kwa wadau tafiti nne zinazohusu usalama wa chakula ikiwemo jinsi ya kuwa na njia mbadala ya uwasilishaji wa chakula cha misaada kwa wenye upungufu wa chakula hasa chenye lishe.
Alisema tafiti nyingine ni namna ya kutazama hifadhi ya chakula ya taifa kujitathmini shughuli zake na majukumu yake hususan uwezo wa kuhifadhi.
Pia kama hifadhi inaweza kusaidia mashirika mengine, kuangalia vibali vya kuagiza chakula kama vinaweza kukidhi matakwa ya usalama wa chakula na kuwa na sera endelevu za kilimo zitakazoangalia usalama wa chakula.

No comments:

Zilizosomwa zaidi