Wednesday, May 14, 2014

HOTUBA YA WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII MHESHIMIWA LAZARO SAMUEL NYALANDU AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2014/201

 UTANGULIZI
1. Mheshimiwa Spika, baada ya Bunge lako Tukufu kupokea taarifa iliyowasilishwa leo hapa Bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali kupokea na kujadili Utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka 2013/14. Aidha, naomba Bunge lako Tukufu lijadili na kupitisha Mpango na Bajeti ya Wizara kwa mwaka 2014/15.
2. Mheshimiwa Spika, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kuwa hapa Bungeni leo. Nichukue fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kunipa dhamana ya kuiongoza Wizara hii yenye jukumu la kusimamia rasilimali za maliasili na malikale; na kuendeleza Utalii. Pia, nampongeza Mheshimiwa Mahamoud Hassan Mgimwa (Mb) kwa kuteuliwa kuwa Naibu Waziri. Aidha, kwa kushirikiana na wafanyakazi na wadau wa sekta hii, nitajitahidi kwa kadiri ya uwezo wangu kusimamia vema uhifadhi na matumizi endelevu ya maliasili na maendeleo ya utalii.
3. Mheshimiwa Spika, napenda kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira ikiongozwa na Mheshimiwa James Daudi Lembeli (Mb) kwa ushirikiano wao thabiti na Wizara yangu. Maoni na ushauri unaotolewa na Kamati, hususan wakati wa kupitia na kuchambua Utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara kwa mwaka 2013/2014 na Mpango na Bajeti kwa mwaka 2014/2015, yameiwezesha Wizara kutekeleza vema majukumu yake.
4. Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuwapongeza kwa dhati Mheshimiwa Mahmoud Thabit Kombo wa Jimbo la Kiembe-Samaki, Zanzibar; Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa wa Jimbo la Kalenga, Iringa; na Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete wa Jimbo la Chalinze, Pwani kwa kuchaguliwa kuwa wabunge. Aidha, natoa pole kwa familia na wananchi wa majimbo ya Kiembe-Samaki, Kalenga na Chalinze kwa kuondokewa na waliokuwa wawakilishi wao Bungeni. Vile vile, natoa pole kwa familia na watanzania wenzetu walioathirika kutokana na majanga mbalimbali yakiwemo mafuriko, ajali za barabarani, wanyamapori wakali na waharibifu na wengine kupoteza maisha. Namwomba Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu mahali pema peponi, Amina.
5. Mheshimiwa Spika, Hotuba yangu imegawanyika katika sehemu kuu mbili. Sehemu ya kwanza ni Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango na bajeti ya Wizara kwa mwaka 2013/2014. Taarifa hiyo imezingatia utekelezaji wa ahadi na maelekezo yaliyotolewa bungeni, utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010-2015 na maagizo mbalimbali ya Viongozi Wakuu wa Serikali. Sehemu ya pili ni Mpango na Bajeti ya Utekelezaji wa Malengo ya Wizara kwa mwaka 2014/2015.
II. MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI KWA MWAKA 2013/2014
6. Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya Wizara kwa mwaka 2013/2014 umezingatia sera, sheria, mikakati ya kitaifa, maelekezo ya Serikali na ahadi za Waziri Bungeni wakati akihitimisha Hotuba yake kuhusu Mpango na Bajeti kwa mwaka 2013/2014. Utekelezaji huo unahusu sekta ndogo za: Wanyamapori; Misitu na Nyuki; Utalii; Malikale; na Uratibu, Utawala na Maendeleo ya Rasilimaliwatu.
SEKTA NDOGO YA WANYAMAPORI
(i) Utekelezaji wa Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori
7. Mheshimiwa Spika, Wizara imekamilisha mapitio ya Kanuni za Usimamizi wa Wanyamapori wa Taifa na Leseni Maalum ya Uwindaji. Kanuni hizi zitaanza kutumika mwezi Juni 2014. Rasimu za Kanuni za Matumizi ya Silaha za Kiraia zinazotumika kwenye uwindaji wa Wanyamapori; na Kanuni za Uchimbaji Madini ndani ya Mapori ya Akiba zitaanza kutumika mwaka 2014/2015. Aidha, Rasimu ya Kanuni za Uanzishaji wa Kikosi cha Ulinzi wa Wanyamapori inaendelea kupitiwa na wadau ili kuiboresha.
(ii) Ushirikishaji Jamii katika Uhifadhi wa Wanyamapori
8. Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa kuongeza ushiriki wa wadau katika usimamizi na kunufaika na rasilimali za wanyamapori, idadi ya Maeneo ya Jumuiya za Uhifadhi wa Wanyamapori (WMAs) zilizoidhinishwa imeongezeka kutoka jumuiya 17 hadi 19. Aidha, Jumuiya za Jamii (CBO) JUHIWANGUMWA - Rufiji, UMEMARUWA – Wanging’ombe na Mbarali, na WAGA – Iringa Vijijini, zimekamilisha baadhi ya hatua za kuanzisha WMA.
(iii) Ulinzi wa Wanyamapori
9. Mheshimiwa Spika, Mwaka 2013/14, siku za doria 54,574 zilifanyika ndani na nje ya Mapori ya Akiba. Watuhumiwa 391 walikamatwa kwa makosa mbalimbali ambapo kesi 277 zilifunguliwa katika mahakama mbalimbali. Kati ya hizo, kesi 123 zenye washitakiwa 164 zimeisha kwa watuhumiwa kulipa faini ya jumla ya Shilingi 75,686,000. Kesi 154 zenye watuhumiwa 227 zinaendelea katika mahakama mbalimbali. Vilevile, nyara za Serikali na bidhaa mbalimbali zilikamatwa. Aidha, kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama, Wizara ilifanya doria maalum nchi nzima (Operesheni Tokomeza) ambapo watuhumiwa 2,085 walikamatwa na jumla ya kesi 839 zilifunguliwa dhidi yao katika mahakama mbalimbali nchini. Maelezo kuhusu nyara za Serikali, vifaa na mali zilizokamatwa wakati wa Doria na Operesheni Tokomeza yako katika aya ya 10 na 11 katika kitabu cha Hotuba.

10. Mheshimiwa Spika, napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa, Wizara kwa kushirikiana na wadau, imeandaa Mkakati wa Kitaifa wa kukabiliana na ujangili na biashara haramu ya nyara. Tarehe 9 – 10 Mei 2014, Wizara kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), na International Conservation Caucus Foundation (ICCF) iliandaa na kufanikisha mkutano wa Kimataifa “Stopping Wildlife Crime & Advancing Wildlife Conservation” “A call for Action”. Katika Mkutano huo, hatua zifuatazo zilichukuliwa:-
(a) Serikali kwa kushirikiana na UNDP imefikia makubaliano ya kuanzishwa kwa Mfuko Maalum wa Kuhifadhi Wanyamapori (Multlateral Antipoaching and Wildlife Busket Fund) utakao simamiwa na UNDP, na kuchangiwa na nchi, Mashirika, na wadau wahisani wa maendeleo.
(b) Washirika wa Maendeleo, wakiwepo UNDP, Ujerumani, Ufaransa, Uingereza, China, Japan, World Bank, Finland na Benki ya Maendeleo ya Africa (ADB), walitia saini makubaliano ya ushirikiano na Serikali kuhusu Uhifadhi na Ulinzi wa Wanyamapori; huku utiaji sahihi huo ukishuhudiwa na Mhe. Mizengo Pinda (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Bibi Hellen Clerk, Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa – UNDP.

(c) Viongozi wa dini walitoa Tamko la kushirikiana na Serikali katika kuwahamasisha waumini wao kote nchini kupinga vitendo vya Ujangili na Biashara haramu ya nyara.
(d) Serikali iliwatunuku “Life Time Archievement Award” watumishi watano wa Idara ya Wanyamapori kwa niaba ya wahifadhi wastaafu nchi nzima. Watumishi hawa na wengine wameyatoa maisha yao kwa uhifadhi wa wanyamapori. Tuzo hizi zitaendelea kutolewa kwa wahifadhi katika sekta yote ya uhifadhi.
(iv) Ulinzi wa Wananchi Dhidi ya Wanyamapori Wakali na Waharibifu
11. Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri za Wilaya iliendesha siku za doria 696 katika wilaya 19 zilizoathirika kutokana na wanyamapori wakali na waharibifu kwa lengo la kulinda wananchi na mali zao dhidi ya wanyamapori wakali na waharibifu. Hata hivyo, watu 11 wamepoteza maisha na jumla ya ekari 4,345.82 za mazao ziliharibiwa na wanyamapori hao katika Wilaya za Busega, Babati, Monduli, Iringa Vijijini, Tabora, Tunduru na Ilemela. Nachukua fursa hii kutoa pole za dhati kwa wote waliofikwa na majanga hayo. Wizara imetoa kifuta machozi cha jumla ya Shilingi 9,200,000 kwa familia za waliopoteza maisha na Shilingi 98,412,750 kama kifuta jasho kwa wananchi walioharibiwa mazao.

(v) Kuboresha Miundombinu, Vitendea Kazi na Huduma
12. Mheshimiwa Spika, mwaka 2013/2014, barabara zenye urefu wa jumla ya kilomita 220 zimekarabatiwa katika Mapori ya Akiba ya Moyowosi-Kigosi Mkungunero na Maswa. Vile vile, kilomita 136 za mipaka zimesafishwa. Kazi nyingine za ujenzi na ukarabati wa miundombinu pamoja na ununuzi wa vitendeakazi ni kama inavyoainishwa katika aya ya 15 na 16 katika kitabu cha Hotuba.
(vi) Uanzishwaji wa Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania
13. Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa, leo tarehe 13/5/2014, nimetia saini AGIZO la kuanzishwa kwa Mamlaka ya Wanyamapori nchini, ikiwa ni utekelezaji wa Sheria ya Wanyamapori Na. 5, ya 2009; na kwamba Mamlaka hii sasa itatangazwa kwenye Gazeti la Serikali na kuanza kazi Julai, 2014. Aidha, naomba kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Wizara imeamua kuwa Makao Makuu ya TAWA yatakuwa katika mji wa Morogoro. TAWA itachukua majukumu yote, isipokuwa yale ya kisera yatakayoendelea kutekelezwa na Idara ndogo ya Wanyamapori.
(vii) Mfuko wa Uhifadhi Wanyamapori Tanzania
14. Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Uhifadhi wa Wanyamapori (TWPF) ulielekeza matumizi yake katika shughuli za kulinda wanyamapori; utafiti na mafunzo; kutoa elimu kwa umma; na kukarabati miundombinu katika mapori ya akiba, vyuo na Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori. Mwaka 2013/14, Mfuko ulikadiria kukusanya Sh. Bilion 16.4. Hadi Machi 2014, makusanyo yamefikia Sh. Bil. 10, sawa na asilimia 61 ya makadirio.
(viii) Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori
15. Mheshimiwa Spika, Mwaka 2013/2014, Taasisi ilifanya sensa sita za kuidadi wanyamapori katika mifumo ya kiikolojia ya Selous-Mikumi; Ruaha-Rungwa; Pori la Akiba Lukwika-Lumesule; West Kilimanjaro na Pori Tengefu la Ziwa Natron; Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori ya Makao; na Ruaha Kusini. Matokeo ya sensa katika mfumo ikolojia wa Selous-Mikumi yamebaini kuwa idadi ya tembo imepungua kutoka 70,406 mwaka 2006 hadi 13,084 mwaka 2013. Aidha, katika mfumo ikolojia wa Ruaha-Rungwa, idadi ya tembo imepungua kutoka 35,461 mwaka 2006 hadi 20,090 mwaka 2013. Taasisi inatarajiwa kuendelea na zoezi la sensa ya Tembo na wanyama wengine nchi nzima kwa mwaka wa fedha ujao.
16. Mheshimiwa Spika, Taasisi kwa kushirikiana na wadau imeandaa mpango kuhusu njia mbadala ya kupunguza madhara yatokanayo na migongano (conflicts) kati ya binadamu na tembo. Aidha, Taasisi imefanya utafiti kuhusu migongano baina ya binadamu na tembo na kutoa elimu ya kupunguza madhara yatokanayo na migongano hiyo katika Wilaya za Serengeti, Bunda, Kilosa, Tunduru na Namtumbo. Majukumu mengine yaliyotekelezwa yameainishwa katika aya ya 19 hadi 21 ya kitabu cha Hotuba.
(ix) Vyuo vya Taaluma ya Wanyamapori
17. Mheshimiwa Spika, mwaka 2013/2014, Vyuo vya taaluma ya wanyamapori vilidahili jumla ya wakurufunzi 1,129, katika vyuo vya:- Mweka wakurufunzi (540) na Pasiansi (400). Aidha, Kituo cha Mafunzo ya Usimamizi wa Maliasili kwa Jamii cha Likuyu - Sekamaganga kimetoa mafunzo ya uhifadhi kwa wananchi 189 kutoka sehemu mbalimbali nchini. Majukumu mengine yaliyotekelezwa yako katika aya ya 22 katika kitabu cha Hotuba.
(x) Shirika la Hifadhi za Taifa na Mamlaka ya Hifadhi Ngorongoro
18. Mheshimiwa Spika, Shirika la TANAPA na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro zimeendelea na utekelezaji wa majukumu yao chini ya sheria zinazosimamia mashirika hayo kama ilivyoelezwa katika kitabu cha Hotuba, aya ya 23 hadi 31.
SEKTA NDOGO YA MISITU NA NYUKI
(i) Utekelezaji wa Sera na Sheria
19. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014 Wizara imeendelea na taratibu za kukamilisha mapitio ya Sera ya Taifa ya Misitu ya mwaka 1998. Aidha, imeanza kukusanya maoni ya wadau kupitia warsha za kikanda ili kufanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Ufugaji Nyuki ya mwaka 1998.
(ii) Vyuo vya Taaluma ya Misitu na Ufugaji Nyuki
20. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014, jumla ya wakurufunzi 239 walidahiliwa kujiunga na vyuo vya taaluma ya misitu na ufugaji nyuki. Chuo cha Mafunzo ya Ufugaji Nyuki kimedahili wakurufunzi 40 na kati yao, 29 wanajigharimia. Chuo kimeboresha miundombinu kwa kukarabati nyumba mbili za watumishi na kuweka mtandao wa mawasiliano. Chuo cha Viwanda vya Misitu kimedahili wakurufunzi 32 na kati yao 25 wamelipiwa ada na Serikali. Vile vile, Chuo kimefanya ukarabati wa mabweni na kununua samani. Chuo cha Misitu Olmotonyi kimedahili wakurufunzi 167 ambao wote wanajigharimia.
(iii) Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania
(a) Kuimarisha Mipaka ya Misitu
21. Mheshimiwa Spika, Wakala ulihakiki mipaka ya misitu kwa kufanya soroveya na kusafisha mipaka yenye urefu wa jumla ya kilometa 2,341 kwenye misitu ya hifadhi 50 ili kudhibiti uvamizi na uharibifu wa hifadhi za misitu. Mipaka hiyo iliwekewa maboya (beacons) 264 na mabango 553 ili kubainisha mipaka na kutoa tahadhari kwa jamii. Zoezi la kuimarisha mipaka liliendeshwa sanjari na kuwaondoa wavamizi kwenye misitu 24 yenye ukubwa wa hekta 9,500. Katika zoezi hilo mifugo 1,200 iliondolewa na nyumba 65, kambi 9 na tanuri 10 za mkaa ziliharibiwa.
(b) Uendelezaji wa Mashamba ya Miti
22. Mheshimiwa Spika, kazi zilizofanyika katika mashamba 16 ya miti hadi kufikia Machi, 2014 ni kama ifuatavyo: kukuza miche 14,288,673; kupanda miti kwenye maeneo yaliyovunwa yenye ukubwa wa hekta 3,905 na maeneo mapya ya hekta 3,443; kupogolea miti kwenye mashamba 11 yenye ukubwa wa hekta 4,366 na kukagua miti yenye mita za ujazo 768,000 katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya uvunaji na kukusanya maduhuli ya kiasi cha Shilingi 27,275,035,840. Aidha, Wakala umeainisha maeneo ya mashamba mapya yenye ukubwa wa hekta 27,000. Maeneo hayo ni Mbizi – Sumbawanga hekta 12,000; Wino – Songea hekta 10,000; Rubare/Kajunguti – Bukoba hekta 2,500; na Kawetire - Mbeya hekta 2,500.
(c) Udhibiti wa Biashara ya Mazao ya Misitu
23. Mheshimiwa Spika, katika kudhibiti uvunaji haramu na biashara ya mazao ya misitu, jumla ya siku za doria 12,436 ziliendeshwa katika maeneo ya nchi kavu na baharini. Doria hizo zilifanyika kwenye misitu ya hifadhi ya asili 17 ikijumuisha hifadhi za mazingira asilia, mikoko na hifadhi za nyuki na manzuki. Vile vile, doria zimefanyika katika misitu isiyohifadhiwa kwenye wilaya 37 na maeneo 40 ya masoko. Katika doria hizo vipande 100,015 vya mbao, mkaa mifuko 48,235 na magogo 8,520 yamekamatwa. Aidha, kiasi cha Shilingi 921,611,439 zilikusanywa kutokana na udhibiti wa biashara ya mazao ya misitu na watuhumiwa 263 waliokiuka sheria walikamatwa. Kati ya hao, 72 walifungwa, 176 walilipa faini, watuhumiwa watatu waliachiwa huru na 12 hukumu hazijatolewa.
24. Mheshimiwa Spika, Wakala umefanya mapitio ya Mwongozo wa Uvunaji Endelevu na Biashara ya Mazao ya Misitu wa mwaka 2007. Mapitio hayo yanalenga kuboresha usimamizi wa uvunaji na biashara ya mazao ya misitu nchini kwa kuweka utaratibu madhubuti na kuongeza uelewa katika kuzingatia sheria na kanuni za misitu.
25. Mheshimiwa Spika, ufafanuzi kuhusu kazi zilizofanyika kudhibiti na kusimamia moto wa msituni, ushirikishwaji jamii katika usimamizi wa rasilimali misitu, uongoaji wa maeneo yaliyoharibika na kuboresha miundombinu katika hifadhi za misitu umeainishwa katika aya ya 37 – 40 katika kitabu cha Hotuba.
(d) Kuendeleza Ufugaji Nyuki
26. Mheshimiwa Spika, mafunzo kuhusu mbinu bora za ufugaji nyuki yametolewa kwa wafugaji nyuki 2,157 kutoka vikundi 330 katika vijiji 91 vya wilaya 20 ili kuboresha uzalishaji wa mazao ya nyuki. Aidha, wafanyabiashara 50 wamepatiwa mafunzo ya kuhakiki ubora wa mazao ya nyuki na taratibu za kufanya biashara ya mazao ya nyuki. Jumla ya mizinga 8,339 imetengenezwa na kusambazwa kwa wananchi waishio karibu na hifadhi za misitu. Kazi nyingine zilizotekelezwa ili kuendeleza ufugaji nyuki zimeainishwa katika aya ya 41 - 43 ya kitabu cha Hotuba.
(iv) Wakala wa Mbegu za Miti
27. Mheshimiwa Spika, Wakala wa Mbegu za Miti umeendelea na jukumu la kuzalisha na kuuza mbegu na miche bora ya miti. Hadi kufikia Machi, 2014 kilo 8,635 za mbegu za miti ziliuzwa nchini kwa Shilingi 107,461,578 na kilo 33 zenye thamani ya Shilingi 5,519,195 zimeuzwa katika nchi za Paraguay na Vietnam. Vile vile, Wakala umeuza miche 126,074 yenye thamani ya Shilingi 126,545,000. Aina ya Mbegu na miche iliyouzwa imebainishwa katika aya ya 44 na 45 ya kitabu cha Hotuba.
(v) Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania
28. Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2013/2014, Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania imeboresha mazingira na miundombinu ya utafiti kwa kuweka samani, vitendea kazi na vifaa vya utafiti katika jengo jipya la Makao Makuu, Morogoro. Vile vile, Taasisi imejenga uwezo wa rasilimali watu kwa kuwawezesha watumishi 14 kujiunga na masomo katika ngazi za shahada (3), Uzamili (4) na Uzamivu (7). Majukumu mengine yaliyotekelezwa na Taasisi yameainishwa katika aya ya 46 - 50 ya kitabu cha Hotuba.
(vi) Mfuko wa Misitu Tanzania
29. Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2013/2014, Mfuko wa Misitu Tanzania ulikadiria kukusanya jumla ya Shillingi 4,561,000,000 kutoka vyanzo vyake. Hadi Machi 2014, Mfuko umekusanya Shilingi 2,281,231,061 sawa na asilimia 50 ya makadirio. Mfuko umepanga kutumia Shilingi 1,776,511,831 kwa ajili ya kufadhili miradi 161 ya wadau wa misitu na ufugaji nyuki ikiwemo miradi mipya 69. Hadi Machi 2014, jumla ya Shillingi 660,816,168 zimetumika kama malipo ya awali na miradi mipya 14 ipo katika hatua ya kusaini mkataba kabla ya kupewa fedha. Aidha, Mfuko umechangia kujenga uwezo kwa kufadhili wanafunzi 15 katika fani ya misitu na nyuki kwa ngazi mbalimbali. Vile vile, Mfuko umewezesha Wakala wa Mbegu za Miti kupitia na kuchapisha nakala 7,500 za Mwongozo wa Upandaji Miti Tanzania.
SEKTA NDOGO YA UTALII
(i) Sera ya Taifa ya Utalii
30. Mheshimiwa Spika, katika kukuza na kuendeleza utalii nchini, Wizara inaendelea na zoezi la kupitia Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 1999. Hadidu za Rejea kwa ajili ya kuandaa sera zimekamilika na kinachoendelea ni taratibu za kumpata Mtaalamu Mwelekezi kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.
(ii) Uendelezaji Utalii
31. Mheshimiwa Spika, katika zoezi la kukusanya takwimu na kufanya soroveya kuhusu watalii nchini, imekadiriwa kuwa, kwa mwaka 2013 watalii 1,135,884 waliingia nchini na kuliingizia Taifa dola za kimarekani bilioni 1.8 ikilinganishwa na watalii 1,077,058 walioingiza mapato ya dola za kimarekani bilioni 1.7 mwaka 2012. Soroveya ya shughuli za biashara za utalii (tourism establishment survey) imebaini kuwa, idadi ya Wakala wa Biashara za Utalii imeongezeka kutoka 1,037 mwaka 2012 hadi 1,103 mwaka 2013. Taarifa za soroveya hizi zitasaidia kujua mwenendo wa mchango wa sekta ya utalii kwenye Pato la Taifa.
(iii) Bodi ya Utalii Tanzania
32. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza Mkakati wa Utangazaji Utalii wa Kimataifa kwa mwaka 2012-2017, Bodi ya Utalii imefanya mikutano katika Mikoa ya Dar-es-Salaam, Mwanza, Iringa, Morogoro na Arusha. Mikutano hiyo imeshirikisha wadau ikiwa ni pamoja na wahariri na waandishi wa habari wa vyombo vya hapa nchini. Aidha, Bodi imekutana na Mabalozi tisa kati ya 11 ambao nchi zao zimetajwa kwenye Mkakati wa Utangazaji Utalii wa Kimataifa kwa lengo la kujadili masuala ya uhamasishaji watalii. Vile vile, Bodi imefanya mikutano na Balozi za Tanzania katika nchi za Uingereza, Ujerumani, Marekani na Uholanzi ili kutambulisha Mkakati huo. Aidha, Mabalozi wa Utalii wa hisani watatu katika nchi ya Marekani na mmoja nchini Australia wameteuliwa. Juhudi zinafanywa kuteua mabalozi wengine watano (5) katika masoko ya Uingereza, Ujerumani, China, Canada na Brazil. Bodi imehudhuria maonesho ya Utalii kwenye nchi 11 na kushiriki ziara za utangazaji (road show). Majukumu mengine yaliyotekelezwa na bodi yameainishwa katika aya ya 54 - 56 ya kitabu cha Hotuba.
(iv) Wakala wa Chuo cha Taifa cha Utalii
33. Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2013/2014, Chuo kimedahili wakurufunzi 242. Kozi ya awali kwa wakurufunzi wasiokuwa na sifa za kutosha kujiunga na chuo imeanza kutolewa ambapo wakurufunzi 18 wamenufaika na utaratibu huo. Aidha, Chuo kwa kushirikiana na Shirika la Kazi Duniani (ILO), Shirikisho la Vyama vya Utalii Tanzania (TCT) na Chama cha Wamiliki wa Hoteli (HAT) kimeanza kutoa mafunzo katika programu ya ‘Apprenticeship’ kwa wakurufunzi 20.
34. Mheshimiwa Spika, ukarabati wa Hosteli za Chuo Kampasi ya Temeke umekamilika na kuongeza uwezo wa kuchukua wanafunzi kutoka 60 hadi 120. Chuo kimenunua vifaa (small operating equipment) kwa ajili ya mafunzo kwa vitendo katika Kampasi ya Bustani ili kuongeza ufanisi na kutoa mafunzo bora.
SEKTA NDOGO YA MAMBO YA KALE
(i) Sera na Sheria
35. Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea na utaratibu wa kurekebisha Sheria ya Mambo ya Kale Sura 333 na marekebisho yake ya mwaka 1979. Taratibu zinaendelea ili kupata ridhaa ya kutunga Sheria mpya ya Mambo ya Kale.
(ii) Utangazaji na Ushirikishwaji wa Jamii
36. Mheshimiwa Spika, Wizara imeandaa vipindi kuhusu vielelezo vya kisayansi, kiutamaduni na kiteknolojia kuhusu chimbuko na maendeleo ya binadamu Tanzania Bara ili kukuza uelewa wa wananchi kutembelea na kushiriki katika uhifadhi wa Malikale. Vipindi hivyo vya zamadamu na utalii wa ndani vimerushwa kupitia vituo vya Televisheni vya TBC1 na Channel Ten. Lengo la vipindi hivi ni kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa malikale, kuhimiza matumizi endelevu na kukuza utalii. Jumla ya vipindi 15 kuhusu Historia na Maendeleo ya Jiji la Dar es Salaam na 10 kuhusu vivutio vya utalii wa malikale vilivyo katika mji wa kihistoria wa Bagamoyo vimetayarishwa na kutangazwa. Aidha, Wizara imefanya uhamasishaji katika shule zilizopo Mkoa wa Iringa na Wilaya ya Bagamoyo. Utaratibu uliotumika ni kupitia shule za msingi, sekondari, vyuo na kufanya mkutano na Wakala wa Utalii.

37. Mheshimiwa Spika, Wizara imetangaza utalii wa urithi wa utamaduni katika maadhimisho mbalimbali ndani na nje ya nchi yakiwemo: Wiki ya Utalii Duniani; Maonesho ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba); na Sherehe za Tamasha la Utalii na Kumbukizi ya Vita vya Majimaji. Aidha, Wizara imeshiriki kuandaa onyesho la kudumu katika balozi za Tanzania nchini China na Ufaransa. Onesho hili limejikita kuonyesha historia ya chimbuko la mwanadamu kwa kupitia vivutio vya utalii katika bonde la Oldupai, Laetoli na Muhula wa zana za Mawe Isimila.
(iii) Uhifadhi wa Malikale
38. Mheshimiwa Spika, katika kupanua wigo wa utalii kupitia urithi wa utamaduni, Wizara imempata mtaalam wa kuandaa michoro ya jengo la Makumbusho ya Laetoli ili kuhifadhi nyayo za Zamadamu. Kutokana na mpangokazi wa mtaalamu mshauri huyo, kazi ya kuandaa michoro ya jengo hilo itakamilika ifikapo mwezi Desemba, 2014. Aidha, umejengwa uzio na kingo za kuzuia maji ya mvua yasiharibu nyayo za zamadamu za Engarasero. Vile vile, vipeperushi vimeandaliwa kwa ajili ya kutangaza eneo hilo.
39. Mheshimiwa Spika, Kazi nyingine zilizofanyika kuhusu uhifadhi na uendelezaji wa rasilimali za malikale, utafiti wa malikale na uhifadhi wa malikale zimeainishwa kwa kina katika aya ya 62 – 64 katika kitabu cha Hotuba.
(iv) Shirika la Makumbusho ya Taifa Tanzania
40. Mheshimiwa Spika, Shirika limesambaza vipeperushi 10,000 katika shule, taasisi na hoteli za kitalii ili kutoa elimu na kuhamasisha wananchi kutembelea makumbusho. Vipindi vya televisheni vya watoto vimerushwa kwa ushirikiano kati ya Shirika, American Garden na Kituo cha Televisheni cha TBC1. Aidha, programu za watoto zinaendelea kufanyika kila Ijumaa ili kuhamasisha watoto kutembelea Makumbusho.
41. Mheshimiwa Spika, Shirika la Makumbusho Tanzania kwa kushirikiana na Makumbusho ya Alcala - Madrid, Spain liliandaa onesho la Chimbuko la Mwanadamu kwa kutumia vielelezo vilivyotokana na utafiti uliofanyika katika bonde la Olduvai, Ngorongoro. Onesho hilo lilizindulia huko Alcala, Madrid, Spain tarehe 10 Februari, 2014 na litachukua muda wa mwaka mmoja na baadaye litarudishwa Makumbusho ya Taifa Februari, 2015. Vile vile, Shirika limekamilisha Jubilei ya miaka hamsini ya ushirikiano wa Tanzania na Sweden; Nyerere Day; na Onesho la baiolojia katika Makumbusho ya Nyumba ya Utamaduni.
URATIBU, UTAWALA NA MAENDELEO YA RASILIMALI WATU
42. Mheshimiwa Spika, katika kuongeza ufanisi na kuboresha utendaji, Wizara imewezesha watumishi 112 kuhudhuria mafunzo mbalimbali. Kati ya hao, watumishi 98 wamehudhuria mafunzo ya muda mfupi na 14 mafunzo ya muda mrefu. Vile vile, Wizara imeajiri watumishi 42 na inategemea kuajiri watumishi 1,342 wa kada za wahifadhi wanyamapori 937; maafisa ufugaji nyuki 50; maafisa misitu 100; na wasaidizi ufugaji nyuki 80. Taratibu za kuwaajiri zinaendelea katika Mamlaka husika na zinatarajiwa kukamilika ifikapo Julai, 2014. Aidha, Wizara imewapandisha cheo watumishi 432 wa kada mbalimbali na watumishi 134 wamethibitishwa kazini. Majukumu mengine yaliyotekelezwa yameainishwa katika aya ya 68 na 69 ya kitabu cha Hotuba.
UKUSANYAJI MADUHULI
43. Mheshimiwa Spika, mwaka 2013/2014, Wizara ilikadiria kukusanya Shilingi 148,971,444,489. Hadi Machi 2014, Wizara imekusanya jumla ya Shilingi 82,086,269,449 sawa na asilimia 55.1 ya makadirio. Miongoni mwa sababu zilizochangia kutofikia lengo ni pamoja na kurudishwa kwa baadhi ya vitalu vya uwindaji kutokana na kupungua kwa wanyama na kuchelewa kuanza kwa Tozo ya Maendeleo ya Utalii.
III. MPANGO WA MAENDELEO NA BAJETI KWA MWAKA 2014/2015
SEKTA NDOGO YA WANYAMAPORI
(i) Uhifadhi, Usimamizi wa Wanyamapori na Ushirikishwaji Jamii
44. Mheshimiwa Spika, mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kuimarisha usimamizi wa rasilimali za wanyamapori ndani na nje ya Mapori ya Akiba kwa kuendesha siku za doria 106,000. Vile vile, miundombinu, vitendea kazi na huduma zitaboreshwa kwa watumishi katika Mapori ya Akiba na Kanda nane za Kikosi Dhidi Ujangili ili watumishi watekeleza kazi zao ipasavyo. Ufafanuzi wa kina kuhusu Barabara zitakazojengwa katika mapori ya akiba, ushirikishwaji wa wananchi katika ulinzi na uhifadhi, gawio la fedha zitokanazo na uwindaji wa kitalii katika Halmashauri na WMAs, na utekelezaji wa mikataba ya kikanda na kimataifa uko katika aya 71-73 ya kitabu cha Hotuba.
(ii) Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA)
45. Mheshimiwa Spika, kuanzishwa rasmi kwa TAWA kunafungua ukurasa mpya katika historia ya Uhifadhi nchini, na kuwapa matumaini mapya wahifadhi wote, na hasa maaskari wa wanyamapori. Kimsingi, uanzishwaji wa Mamlaka umezingatia haja ya kujenga uwezo, kuboresha maslahi ya watumishi na kuimarisha shughuli za uhifadhi kwenye mapori ya akiba na maeneo yote nje ya TANAPA na NCA.
46. Mheshimiwa Spika, Chini ya Mamlaka ya Wanyamapori, tunaongeza vitendea kazi ili kuimarisha ulinzi na doria, na kuhakikisha tunawashinda majangili popote nchini. Tunaanzisha Kitengo Maalum cha doria za Helikopta kwa ajili ya kuwalinda wanyamapori, hususani Tembo na Faru kama ifuatavyo:-
(a) Selous Game Reserve – Helikopta moja aina ya Robertson 44 inayonunuliwa kwa ufadhili wa Taasisi ya Howard Buffet;
(b) Ngorongoro Conservation Area – Helikopta aina ya Robertson 44; na
(c) Helikopta aina ya Bell, inayonunuliwa na TANAPA. Marubani 6 kwa ajili ya Helikopta wanaanza mafunzo nchini Afrika Kusini mwishoni mwa mwezi huu.
47. Mheshimiwa Spika, ili kufanikisha ulinzi wa Tembo, Wizara inaanzisha kitengo maalum cha mafunzo ya Inteligensia na ukomandoo wa Kikosi maalum kitakachokuwa na uwezo wa kuteremka kwenye helikopta katikati ya pori na kuwatia nguvuni majangili. Aidha, Chuo cha Maaskari wa Wanyamapori Pasiansi, kupitia Taasisi ya Howard Buffet, kinapata miundombinu mipya ya mabweni ya wananfunzi 300 zaidi, GPS, Darubini, Mabasi maalum 2, malori maalum 2, magari 5 mahema ya mafunzo, mtaalam mwelekezi, pamoja na kujengewa uwezo kumudu mahitaji maalum ya Taaluma hii kulingana na changamoto za wakati huu.
48. Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania itasimamia eneo lenye ukubwa wa kilometa za Mraba 200,000, ikiwepo Mapori yote ya Akiba (28) na Mapori Tengefu (43). Shirika la Hifadhi za Taifa litaendelea kusimamia hifadhi 16 zenye jumla ya ukubwa wa kilometa za mraba 57,000 na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro itaendelea kusimamia eneo lake la kilometa za mraba 8,500.

49. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwisho wa mwezi ujao, Wizara itakuwa na jumla ya Askari wa Wanyamapori 2,532, walio chini ya Mamlaka nilizozitaja hapo juu.
50. Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Kuhifadhi Wanyamapori (TWPF) ulio chini ya Wizara, pamoja na Mfuko wa wadau wa maendeleo ulio chini ya UNDP (Multilatoral Antipoaching and Wildlife Security Busket Fund) pamoja na rasilimali zingine zitatumika kuijengea Mamlaka ya Wanyamapori uwezo wakati tunaianzisha, Makao yake Makuu yakiwa Mjini Morogoro. Nia na Azma ya Serikali ni kuhakikisha kuwa hatua hizi za kuanzisha mfumo mpya wa Mamlaka utaweza kulinda rasilimali za nchi, na kuhakikisha uwepo wa Tembo na Wanyamapori wengine katika miaka mingi ijayo.
51. Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania itakuwa na Bodi inayojitegemea, na itakuwa na Mkurugenzi Mkuu (Director General) atakayeteuliwa na Mhe. Rais, na itakuwa na vyanzo vyake vya mapato vitakavyoainishwa katika mabadiliko ya sheria.
(iii) Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori
52. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/2015, Taasisi itaendeleza utafiti wa wanyamapori, aina za nyuki, mahusiano kati ya nyuki na mimea pamoja na kuidadi wanyamapori katika maeneo mbalimbali ya nchi. Mafunzo kuhusu njia stahiki za ufugaji nyuki yatatolewa katika vijiji vya Wilaya za Simanjiro, Kiteto na Hanang na kutengeneza mizinga 1,500 kwa ajili ya kuisambaza kwa wadau wa sekta ya ufugaji nyuki. Aidha, Taasisi itaendelea na ujenzi wa maabara ya utafiti wa nyuki.

(iv) Vyuo vya Taaluma ya Wanyamapori
53. Mheshimiwa Spika, vyuo vya mafunzo ya uhifadhi wanyamapori vitadahili jumla ya wakurufunzi 980: Pasiansi - 400 na Mweka - 580. Kituo cha Mafunzo ya Usimamizi wa Maliasili kwa Jamii - Likuyu Sekamaganga kitatoa mafunzo kwa wananchi 240. Vile vile, Chuo cha Mweka kitawezesha wakufunzi watatu kupata mafunzo ya Uzamili na wawili Uzamivu. Aidha, Chuo kitajenga madarasa mawili na matanki matatu yenye jumla ya mita za ujazo 450 kwa ajili ya kuhifadhi maji.

(v) Shirika la Hifadhi za Taifa, Tanzania
54. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/2015 Shirika litaendelea kutatua migogoro ya mipaka na shoroba; na kuimarisha mifumo ya TEHAMA. Vilevile, Shirika litaboresha miundombinu ya majengo, madaraja, barabara, maliwato ya mlimani, nyumba za wafanyakazi, huduma ya maji, na umemejua. Pia, Shirika litaimarisha utalii na kupanua wigo wa vivutio na huduma kwa watalii, kuajiri watumishi ikiwa ni pamoja na kuwa na muundo wa ‘Paramilitary’ ili kuimarisha uhifadhi.
55. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza kazi hizo, Shirika litanunua vifaa vya kisasa ikiwa ni pamoja: silaha, vifaa vya mawasiliano ya ki-intelijensia, na vifaa mbalimbali vya kuboresha ufuatiliaji wa karibu wa Faru kwa ajili ya kudhibiti ujangili. Vile vile, Shirika litanunua Helikopta, aina ya Bell, magari 12, na mitambo mizito ya barabara miwili. Aidha, Shirika litaweka mifumo mipya 12 ya ki-elektroniki ya kukusanya mapato katika Hifadhi saba, kujenga/kukarabati nyumba 15 za watumishi na kuweka seti 21 za umemejua katika vituo vya maaskari. Vile vile, Kituo cha Utalii kitajengwa katika Hifadhi ya Arusha. Pia, mabanda manne ya kulala Watalii wa ndani yatajengwa katika Hifadhi za Ruaha na Saadani. Vituo vinne vya kupumzikia wageni na mabanda mawili ya wapagazi (Porters) yatajengwa katika Hifadhi ya Kilimanjaro. Jumla ya Kilometa 26 za barabara mpya zitajengwa katika Hifadhi ya Mikumi. Aidha, Shirika litajitangaza vivutio vya utalii kupitia televisheni za ndani na za kimataifa kama vile CNN, CCTV na CNBC.
(vi) Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro
56. Mheshimiwa Spika, Mwaka 2014/2015, Mamlaka itaendelea kununua na kusambaza chakula kwa wafugaji waishio ndani ya Hifadhi ambapo tani 4,700 za mahindi zitatolewa. Shule za msingi 21 zimetengewa Shilingi 70,000,000 kwa ajili ya kununua chakula. Vile vile, Mamlaka itanunua helkopta moja, magari 10, basi moja la utalii wa ndani, gari la kutoa huduma kwa wagonjwa, kujenga nyumba mbili za askari katika vituo vya Lemala na Selela na kukarabati nyumba nne za maaskari katika vituo viwili. Mamlaka pia itaimarisha doria kwa kununua na kutumia zana mbalimbali za kisasa na kuendelea na ujenzi wa jengo la kitega uchumi Jijini Arusha. Majukumu mengine yatakayotekelezwa yameainishwa katika aya ya 79 hadi 81 ya kitabu cha Hotuba.
SEKTA NDOGO YA MISITU NA NYUKI
(i) Sera na Sheria
57. Mheshimiwa Spika, rasimu ya Sera ya Taifa ya Misitu imekamilika na taratibu za kuidhinishwa zinaendelea. Mapitio ya Sera ya Taifa ya Ufugaji Nyuki yataendelea kwa kukusanya maoni ya wadau. Kufuatia kukamilika kwa mapitio ya Programu ya Taifa ya Misitu ya 2001 - 2010 utayarishaji wa programu mpya utaendelea. Aidha, uchambuzi wa Sheria ya Misitu Sura 323 na Sheria ya Ufugaji Nyuki Sura 224 utafanyika ili kuainisha majukumu ya Wakala wa Huduma za Misitu.
(ii) Vyuo vya Taaluma ya Misitu na Ufugaji Nyuki
58. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/2015, Jumla ya wakurufunzi 308 watadahiliwa kama ifuatavyo: Chuo cha Misitu Olmotonyi 195, Chuo cha Viwanda vya Misitu 40 na Chuo cha Mafunzo ya Ufugaji Nyuki 73. Katika kuboresha miundombinu, Chuo cha Viwanda vya Misitu kitajenga maktaba na maabara. Chuo cha Misitu Olmotonyi kitafanya ukarabati wa nyumba tisa za watumishi, ukumbi wa mikutano, bwalo la chakula na kiwanda cha kupasua mbao. Chuo cha Mafunzo ya Ufugaji Nyuki kitajenga nyumba moja ya waalimu na karakana ya mbao pamoja na kukarabati jengo la utawala na kuliwekea samani.
(iii) Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania
59. Mheshimiwa spika, katika mwaka 2014/2015, Wakala utaanza kutekeleza Mpango Mkakati wa miaka mitano (Julai 2014 - Juni 2019). Mpango huu umelenga kuendeleza rasilimali za misitu na nyuki na kuboresha mifumo ya usimamizi. Aidha, Mpango wa Kibiashara kwa mwaka 2014/2015 unaosisitiza kuimarisha uwezo wa Wakala katika kutoa huduma, upatikanaji wa rasilimali na mifumo ikolojia pamoja na kuwezesha matumizi ya rasilimali zilizoboreshwa utatekelezwa.
(a) Usimamizi wa Rasilimali za Misitu na Nyuki
60. Mheshimiwa Spika, ili kuimarisha usimamizi wa rasilimali za misitu na kudhibiti uvunaji haramu wa mazao ya misitu, Wakala unatarajia kuendesha siku za doria 22,000 katika maeneo mbalimbali nchini. Kamati za uvunaji katika Halmashauri 55 za wilaya zitawezeshwa kufanya vikao vya kujadili maombi ya uvunaji. Vile vile, Wakala utafanya mikutano 14 kwa wafanyabiashara wa mazao ya misitu na nyuki katika Kanda za Kaskazini, Kusini, Mashariki, Kati na Ziwa. Lengo la mikutano hiyo ni kuelimisha wafanyabiashara kuhusu sheria na taratibu za kufanya biashara ya mazao ya misitu. Majukumu mengine yatakayotekelezwa yameainishwa katika aya ya 86 hadi 88 ya kitabu cha Hotuba.
(b) Usimamizi wa Mashamba ya Miti
61. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/2015, jumla ya miche 15,000,000 itaoteshwa na kupandwa katika mashamba ya miti yenye ukubwa wa hekta 7,300. Wakala utarudishia miti katika maeneo yenye ukubwa wa hekta 200; utaondoa magugu kwenye eneo la hekta 33,150, kupogoa hekta 1,812 na kukarabati barabara za msituni zenye urefu wa jumla ya kilomita 2,691. Aidha, usimamizi wa mashamba ya miti utafanyika kwa kufanya doria kwenye eneo la hekta 214,000, kusafisha barabara za kuzuia moto zenye urefu wa kilomita 6,120 na kusafisha mipaka kilomita 862.
62. Mheshimiwa Spika, Katika kupunguza changamoto ya uhaba wa malighafi ya mazao ya misitu, Wakala utaanzisha mashamba mapya yenye ukubwa wa jumla ya hekta 2,225 ya spishi za aina mbalimbali. Vile vile, eneo la msitu wa asili Kahe – Kilimanjaro hekta 50 litapandwa misaji na shamba la nishati ya kuni lililopo Korogwe hekta 50 litapandwa mikaratusi. Aidha, Wakala unatarajia kuanzisha hekta 50 za mikaratusi na mianzi katika Msitu wa Hifadhi wa Ruvu. Kazi nyingine za usimamizi wa rasilimali za misitu, ushirikishaji jamii, elimu kwa umma, kuwajengea wwatumishi uwezo zimeainishwa katika aya ya 85 hadi 93 ya kitabu cha Hotuba.
(c) Kuanzisha Vituo vya Kuzalishia Makundi na Kuendeleza Ufugaji Nyuki
63. Mheshimiwa Spika, Katika kukabiliana na upungufu wa makundi ya nyuki unaosababishwa na mabadiliko ya tabia nchi, Wakala utaanzisha vituo vitano vya kuzalishia malkia wa nyuki. Vituo hivyo ni: NAFRAC – Shinyanga, Ukimbu – Manyoni, Ruvu – Kibaha, Nandembo – Tunduru na Shamba la Miti Sao Hill. Aidha, Wakala utatoa mafunzo ya uzalishaji wa makundi ya nyuki kwa wawezeshaji 40. Kati ya watakaopewa mafunzo 20 ni watumishi na 20 wanatoka kwa wawakilishi wa wafugaji nyuki. Wakala utatoa mizinga 1,200 na mafunzo kwa wafugaji nyuki kutoka vijiji 91 vilivyoko kandokando ya misitu. Jumla ya wafugaji nyuki 1,501 kutoka vikundi 115 watanufaika na mafunzo hayo.
(d) Kongamano la Ufugaji Nyuki – APIMONDIA

64. Mheshimiwa Spika, ninayo furaha kulitaarifu Bunge lako tukufu kuwa kwa mara ya kwanza barani Afrika, Tanzania imepata heshima ya kuandaa Kongamano la Ufugaji Nyuki (APIMONDIA). Lengo ni kuongeza msukumo wa ufugaji nyuki na kupanua wigo wa masoko ya mazao ya nyuki. Kongamano litafanyika tarehe 11 hadi 13 Novemba, 2014 katika ukumbi wa Kituo cha Mikutano ya Kimataifa wa AICC, Arusha. Jumla ya washiriki 550 kutoka ndani na nje ya nchi wanatarajiwa kuhudhuria. Kongamano hilo litaambatana na maonesho ya kibiashara na ziara za mafunzo.
(iv) Wakala wa Mbegu za Miti
65. Mheshimiwa Spika, Ili kuhakikisha kuwa upatikanaji wa mbegu bora za miti unakuwa endelevu, Wakala utaanzisha vyanzo vitano vya mbegu bora za miti ya Misindano aina mbili, Msenefu, Mwiluti na Mpaulonia. Vilevile, Wakala utatambua na kusajili vyanzo vitatu vya mbegu za miti aina ya Mkenge na Mgunga. Pia, utaendelea kutunza vyanzo 31 vya mbegu za miti ya aina mbalimbali. Wakala utakusanya jumla ya kilo 12,500 za mbegu ya miti aina mbalimbali pamoja na kuuza kilo 11,500 za mbegu za miti na miche ya miti 100,000.
(v) Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania
66. Mheshimiwa Spika, kutokana na wakulima wengi kuvuna miti yao katika umri mdogo na hivyo kupoteza mapato, Taasisi itafanya utafiti juu ya ubora wa mbao zitokanazo na miti ya umri tofauti. Lengo ni kutoa ushauri wa kisayansi juu ya umri stahiki wa kuvuna miti bila kuathiri ubora wa mbao kwa matumizi mbalimbali .Aidha, taasisi itaanzisha mashamba darasa katika Wilaya za Mkuranga na Handeni ili kuelimisha jamii inayozunguka misitu ya hifadhi juu ya umuhimu wa kuwa na mashamba ya miti ya kuni na matumizi mengine. Aidha, Taasisi itaajiri watafiti wasaidizi tisa, watafiti waandamizi watano, wakurugenzi wa vituo vya utafiti wanne na watumishi wengine 27 pamoja na kununua samani na vitendea kazi vya ofisi na maabara.
(vi) Mfuko wa Misitu Tanzania
67. Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Misitu Tanzania unakadiria kukusanya jumla ya Shilingi 5,357,540,000 kutokana na vyanzo vyake vya mapato. Mfuko utatoa ufadhili wa Shilingi 1,992,603,7000 kwa ajili ya miradi 173 ya wadau mbalimbali wa misitu na ufugaji nyuki. Kati ya miradi hiyo 97 ni mipya. Wadau watakaonufaika na ufadhili wa Mfuko ni pamoja na watu binafsi, vikundi vya jamii, asasi za kiraia, taasisi zisizo za Kiserikali na taasisi za Serikali zikiwemo Serikali za Mitaa.
SEKTA NDOGO YA UTALII
(i) Sera na Sheria
68. Mheshimiwa Spika, Wizara itafanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Utalii ya mwaka 1999 ili iendane na mahitaji halisi katika sekta ya utalii. Maandalizi ya sera mpya yatazingatia hatua zote muhimu kwa kushirikisha wadau kupitia mikutano. Aidha, itafanya warsha kwa wadau wa utalii katika kanda nne ili kuhamasisha utekelezaji wa Kanuni za utalii.
(ii) Uendelezaji wa Utalii
69. Mheshimiwa Spika, Wizara itaendelea kufanya utafiti wa mwenendo wa biashara ya utalii nchini pamoja na kukusanya na kuainisha takwimu za utalii. Kazi ya kukagua wakala wa biashara za utalii itafanyika katika kanda nne ambazo ni Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Pwani, Kanda ya Nyanda za juu Kusini na Kanda ya Ziwa. Vile vile, Wizara itaainisha vivutio vya utalii katika mikoa ya Singida na Katavi na kutoa ushauri wa kitaalamu wa kuviboresha.
(iii) Bodi ya Utalii Tanzania
70. Mheshimiwa Spika, nachukua fursa hii kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa kuanzia mwezi wa Julai, 2014, tunachukua hatua madhubuti za kuhuisha mtazamo wa dunia juu ya Taifa letu na Utalii nchini Tanzania. Bodi ya Utalii, kwa kushirikiana na Shirika la Hifadhi za Taifa TANAPA, na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro itasimamia kutangazwa kwa vivutio vya Utalii vilivyopo katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika matangazo maalum ya Runinga yatakayoanza kurushwa katika vituo vya CNN na BBC kwa kipindi cha mwaka mzima. Aidha, tunatarajia kumwomba Mheshimiwa Rais azindue “Mpango wa Kuhuisha Mtazamo wa Dunia Kuhusu Utalii Tanzania”. (Re-Branding Destination Tanzania mapema mwezi Julai, 2014).
71. Mheshimiwa Spika, Bodi itashiriki maonesho na misafara ya utangazaji ya utalii ya Kimataifa itakayofanyika katika nchi za Uholanzi, Hispania, Ujerumani, Uturuki, Uingereza, China, Urusi, Afrika ya Kusini, India, Brazil, Italia na Nchi za Ghuba. Aidha, Bodi itatumia mitandao ya kijamii kutangaza vivutio vya utalii. Mikakati mingine itahusisha kuandaa Tamasha la Utalii wa Utamaduni kwa kushirikiana na Chuo cha Sanaa cha Bagamoyo; kuandaa safari mbili za kupanda Mlima Kilimanjaro; kutangaza utalii kupitia michezo; na kuendesha onesho jipya la Kimataifa la Utalii (Swahili International Tourism Exhibition). Vile vile, Bodi itafungua ofisi za uwakilishi kwa ajili ya kutangaza utalii nchini India na Ujerumani na kuendelea kuimarisha ofisi ya uwakilishi iliyoko nchini Marekani (the Bradford Group).
72. Mheshimiwa Spika, Bodi itaendelea kutangaza utalii wa ndani kupitia Maonesho sita ambayo ni Sabasaba, Nanenane, Karibu Travel Fair, Siku ya Utalii Duniani, Tamasha la Kimataifa la Filamu la Zanzibar na Tamasha la Sauti za Busara.
(iv) Wakala wa Chuo cha Taifa cha Utalii
73. Mheshimiwa Spika, Chuo kitadahili Wakurufunzi 312 kwa mwaka 2014/2015 na wakurufunzi 50 wa kozi ya awali kwa wasiokuwa na sifa za kutosha kujiunga na Chuo ngazi ya Astashahada. Aidha, Chuo kupitia mradi unaofadhiliwa na Serikali ya Uswisi chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, kitaanzisha mafunzo ya wawezeshaji (Training of Trainers) kwa ajili ya wakufunzi wa vyuo vya Hoteli na Utalii. Pia, utafanyika upembuzi yakinifu kwa ajili ya ujenzi wa madarasa na maktaba katika Kampasi ya Arusha.
SEKTA NDOGO YA MALIKALE
74. Mheshimiwa Spika Wizara itafanya mapitio ya Sheria ya Malikale na kuandaa miongozo ya utafiti na uhifadhi wa Malikale katika maeneo ya kihistoria ya Kilwa Kivinje, Mikindani na Mji wa Kihistoria Pangani. Aidha, Wizara itafanya ukarabati wa Boma la Pangani na jengo la zamani la Mahakama Kalenga Iringa; ujenzi wa kituo cha taarifa cha Amboni Tanga; ujenzi wa uzio katika Kituo cha Kunduchi; na kuboresha mandhari ya kituo cha Ujiji Kigoma na Kaole Bagamoyo. Wizara itaandaa orodha ya maeneo ya wapigania uhuru katika Mkoa wa Mtwara. Vile vile, itashiriki mikutano ya kitaalamu ngazi ya Kimataifa ili kunufaika na fursa zilizopo.
(i) Shirika la Makumbusho ya Taifa
75. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2014/2015, Shirika litaendelea kuitangaza Makumbusho kwa kutumia vipindi vya televisheni, redio, mitandao ya kijamii, vipeperushi na kupitia maonesho mbalimbali ya ndani na nje ya nchi. Aidha, litajenga uwezo kwa watumishi na kuboresha mazingira ya kazi kwa vituo vya Arusha, Musoma, Ruvuma na Dar es Salaam. Vile vile, Shirika litaongeza vituo vya makumbusho Chamwino, Singida na Mwanza pamoja na kufanya upanuzi katika vituo vya Butiama na Elimu viumbe Arusha. Shirika pia litaratibu Tamasha la Utamaduni wa Mtanzania litakaloshirikisha jamii kutoka Mkoa wa Kagera.
URATIBU, UTAWALA NA MAENDELEO YA RASILIMALI WATU
76. Mheshimiwa Spika, Wizara itawezesha watumishi 846 kuhudhuria mafunzo ya muda mfupi na mrefu. Aidha, Wizara itapandisha cheo watumishi 522 na kuaajiri 1,033 (641 kada ya Wahifadhi Wanyamapori na 322 kada ya Misitu). Vilevile, watumishi watawezeshwa kupata mikopo kutoka Mfuko Mkuu wa Serikali na Benki binafsi; Watumishi wanaoishi na virusi vya UKIMWI wataendelea kupokea huduma ya lishe. Wizara itaimarisha Chama cha Kuweka na Kukopa (MNRT SACCOS) pamoja na kuendelea kuratibu upatikanaji wa mikopo kwa watumishi wake kutoka Mfuko Mkuu wa Serikali na Benki binafsi. Majukumu mengine yatakayotekelezwa yameainishwa katika aya ya 107 na 108 ya kitabu cha Hotuba.
IV. SHUKURANI
77. Mheshimiwa Spika, shukurani zangu za dhati napenda ziende kwa Mheshimiwa Mahamoud Hassan Mgimwa (Mb) Naibu Waziri, Mbunge wa Mufindi; Bibi Maimuna Kibenga Tarishi, Katibu Mkuu na Bwana Selestine Gesimba, Naibu Katibu Mkuu. Vile vile, nawashukuru Wakuu wa Idara na Vitengo, Mashirika, Wakala, Taasisi na Vyuo pamoja na watumishi wa Wizara ya Maliasili kwa kujitoa kwa dhati katika kutekeleza majukumu ya Wizara.
78. Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa hii kuwashukuru wote walioshiriki kuiwezesha Wizara kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Nianze kwa kuwashukuru washirika wa maendeleo ambao ni pamoja na nchi wahisani, mashirika ya misaada, taasisi zisizo za Kiserikali na taasisi za fedha. Kwa namna ya pekee, napenda kuwataja baadhi yao kama ifuatavyo: Serikali za: Marekani, Uingereza, China, Finland, Norway, Ubelgiji, Ufaransa na Ujerumani; Jumuiya ya nchi za Ulaya; Mashirika ya Umoja wa Mataifa ya FAO, ICCROM, UNDP-GEF, UNESCO na UNWTO; WB, na Mashirika ya misaada na taasisi zisizo za kiserikali za AWF, AWHF, BTC, DANIDA, FZS, GIZ, ICOMOS, IUCN, KfW, LATF, USAID, WMF, WHC, WWF, na Kipekee, Taasisi ya HBF.
V. HITIMISHO
79. Mheshimiwa Spika, Katika mwaka 2014/2015, naomba Bunge lako Tukufu likubali kupitisha makadirio ya matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii ya jumla ya Shilingi 83,119,264,000. Kati ya hizo, Shilingi 68,921,048,000 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi 14,198,216,000 ni kwa ajili ya Miradi Maendeleo. Fedha za Matumizi ya Kawaida zinajumuisha Shilingi 30,627,417,000 kwa ajili ya Mishahara ya watumishi na Shilingi 38,298,631,000 kwa ajili ya Matumizi Mengineyo. Fedha za Maendeleo zinajumuisha Shilingi 5,000,000,000 fedha za ndani na Shilingi 9,198,216,000 fedha za nje.
80. Mheshimiwa Spika, Naomba kutoa Hoja.

No comments: