Sunday, September 22, 2013

SIASA ZA CCM ZAMPONZA BALOZI WA CHINA

 
SIKU chache baada ya Balozi wa China nchini, Lu Youqing, kukiuka mkataba wa kimataifa wa Vienna kwa kushiriki kazi ya uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Tanzania Daima limedokezwa kuwa kuna harakati za kumrudisha nyumbani kwao.
Septemba 12 mwaka huu, balozi huyo alihudhuria mkutano wa hadhara wa CCM uliofanyika uwanja wa Shycom mkoani Shinyanga na baadaye katika eneo la mnada wa Mhunze Jimbo la Kishapu.
Balozi Youqing alitambulishwa kwa wananchi waliofika kwenye mkutano huo na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, na alihutubia akisema China imevutiwa na sera za chama hicho na hivyo itawekeza katika soko la pamba katika mkoa huo.
Tukio hilo limeitia doa Serikali ya China ambayo licha ya ‘urafiki’ na Serikali ya CCM, imekuwa ikilaumiwa kwa kukiuka haki za binadamu na mataifa mbalimbali ulimwenguni.
Balozi huyo amezusha maswali mengi miongoni mwa jamii juu ya uelewa wake wa masuala ya kimataifa, hasa mkataba Vienna wa mwaka 1961 kifungu cha 41(1) kinachozungumzia uhusiano wa kidiplomasia.
Kifungu hicho kinazuia balozi yeyote kujihusisha na siasa kwenye nchi anayofanyia kazi.
Katika mkutano huo, balozi huyo alicheza nyimbo za CCM za kubeza vyama vya upinzani huku akiwa amevalia kofia ya chama hicho tawala.
Wachambuzi wa masuala ya diplomasia wamekuwa na mtazamo wa aina mbili juu ya tukio hilo lililotia doa Serikali ya China na CCM.
Mtazamo wa kwanza ni kuwa viongozi wa CCM wakiongozwa na Kinana walilenga kumtumia balozi huyo kutafuta uungwaji mkono na wananchi wa Shinyanga.
Wanabainisha kuwa balozi huyo ameingizwa ‘mkenge’ na CCM inayojipatatua kurejesha imani yake kwa wakazi wa Kanda ya Ziwa ambao wanaonekana kuviunga mkono vyama vya upinzani.
Mtazamo wa pili wa wachambuzi hao ni juu ya elimu na uzoefu wa balozi huyo katika masuala ya kimataifa kiasi cha kushindwa kubaini kile alichokuwa akikifanya ni kosa.
Maofisa wa ubalozi wa China hapa nchini wameelezea hatua atakazochukuliwa balozi huyo, lakini hawakuwa tayari kuzungumzia jambo hilo.
Ofisa mmoja ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini, alisema mzungumzaji wa masuala ya kibalozi ni balozi ambaye hayupo tayari kulizungumzia.
Inadaiwa ushiriki wa balozi huyo kwenye shughuli za CCM umewashtua mabalozi wengine ambao wameweka wazi kuwa kabla ya kupangiwa vituo vyao vya kazi hupewa mafunzo maalumu ya mambo ya kufanya pamoja na mikataba ya kimataifa. 

No comments:

Zilizosomwa zaidi