Tuesday, August 5, 2014

HII NI MPYA, MLEMAVU ATUHUMIWA KUUZA UNGA



Jeshi la Polisi Kanda Maalumu Dar es Salaam, limemkamata mkazi wa Vijibweni, Said Tindwa kwa kosa la kufanya biashara ya dawa za kulevya aina ya cocaine na heroine.
Kamanda wa kanda hiyo, Kamishna Suleiman Kova alisema mtuhumiwa huyo ambaye ni mlemavu anayetumia mguu bandia, amekuwa akiutumia vibaya kwa kuficha dawa ndani yake na kuwauzia watumiaji.
Alisema mtuhumiwa huyo aliweka dawa hizo kwenye pakiti na kuziuza sehemu mbalimbali kwa Sh1,000.
“Tulimkamata Agosti 2 mwaka huu katika mtego maalumu uliowekwa na askari wa upelelezi,” alisema Kova.
Alisema uchunguzi wa awali ulibaini kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa akitumia mbinu hiyo kwa muda mrefu kabla ya kukamatwa.
Kova alisema dawa alizokuwa akiuza mtuhumiwa ni zile za viwandani kama cocaine, heroine na bangi.
Wakati huohuo, polisi wanamshikilia askari polisi aliyerusha bomu la machozi, Mbagala Zakhiem na kumjeruhi mkazi mmoja wakati wakimsaka mtuhumiwa wa wizi wa pikipiki.
Aliyepigwa na bomu hilo ni Mwanaharusi Hamis ambaye amelazimika kukatwa kiganja cha mkono wa kulia baada ya kujeruhiwa vibaya.
Mwanaharusi alilipuliwa na bomu hilo Agosti Mosi mwaka huu, saa 3 usiku akiwa nyumbani kwake na sasa amelazwa Hospitali ya Taifa Muhimbili.

No comments:

Zilizosomwa zaidi